Professional Documents
Culture Documents
Mara nyingi Zanzibar imejaribu kujipatiya utulivu na haikuweza kufaulu. Haya yalitokeya kabla ya Mapinduzi
na yakajaribiwa tena baada ya Mapinduzi na zaidi kwenye Miafaka ya hivi karibuni. Wakati wa Mwenye Enzi
Mungu kutaka ulikuwa bado haukufika na pia kwa sababu ya mashindano ya kisiasa baina ya Wazanzibari
wenyewe kwa wenyewe yanayotokana na tabia ya kutoaminiyana.
- Harith Ghassany katika kitabu chake - Kwaheri Uhuru Kwaheri Ukoloni
----------------------
Mabadiliko ya zama na mabadiliko ya fikra huwa ni wimbi. Wimbi ambalo mara likiingia katika mzunguko
wake hakuna anayeweza kulizuia kwa sababu wimbi husonga mbele kwa maumbile yake na hupambana na kila
kipingamizi kinachozuia safari yake.
Ally Saleh – katika makala “ Siasa na migogoro
Zanzibar: Fikra mpya katika zama mpya”
Utangulizi.
Visiwa vya Zanzibar na Pemba si vigeni kabisa katika medani ya siasa na migogoro. Tunaweza kusema ni
mwenyeji kwa kiasi kikubwa ingawa kwa udogo wake hali hizo za siasa na migogoro inafanana na udogo
wake.
Visiwa hivi vimepita katika vipindi vingi vya aina hiyo na kuibuka na michubuko na majeraha lakini kila siku
vikasonga mbele ila tatizo likawa vimeshindwa kusahau na kila mara kovu za hayo zikawa zinaibuka
kukumbushia.
Visiwa hivi vimepoteza maisha mengi, mali nyingi na muda mwingi wakati vikichanja mbuga katika siasa na
migogoro ya kisiasa kuanzia ambayo msingi wake ni ukabila na rangi mpaka ile ambayo misingi yake ni
kuwania madaraka na hata ubinafsi.
Muda wa kupita katika matukio hayo ulianzia ule ambao vyama vilikuwa bado katika uchanga wake na vikiwa
vinaenda tata, hadi vilipoanza kukua na kuingia katika harakati za kiuchaguzi mpaka kufikia kubaleghe na
kuingia kwenye mchakato wa kudai uhuru.
Muundo wa vyama hivyo tokea awali ulikuwa na kasoro, lakini kasoro ambazo leo ndio tunaweza kuiona
tukitizama nyuma lakini wakati huo haingewezekana kuziona na ndio maana mengi yalitokea bila ya kuweza
kuzuilika Hata utawala wa Kisultani na Kiingereza nao ulikuwa na mtizamo ambao haukuwa muwafaka
kuweza kuwa na ushindani wa kisiasa ambao ungekuwa na lengo la kuisha kwa salama na amani bali ulikuwa
ule ambao siku zote ungeweza kujenga zaidi uadui kuliko masikilizano.
Ila baya tunaloweza kulisema hata katika kipindi ambacho chama kilikuwa ni kimoja lakini bado siasa za
chuki, kukumbushana yaliopita vilikuwa ni vitu vilivyoendelezwa na kiasi kuwa na chama kimoja hakukusaidia
lolote katika kupata maridhiano.
Na baya zaidi ni ule kuona hata katika kurudisha mfumo wa vyama vingi vya siasa hapo mwaka 1992 bado
hatukuweza kuepuka mfumo na utaratibu ule wa kuwa na vyama ambavyo macho na akili za vyama hivyo
vilirudi kule kule katika siasa za malumbano, kutengana na kubaguana.
Sasa ni miongo miwili katika siasa za ushindani wa vyama na tunaelekea kuwa na uchaguzi wa nne, ufa katika
ukuta wa Zanzibar haujazibika na kuna wakati mwingi ufa huo umetishia kupanuka na kuashiria hatari zaidi.
Tumeambizana na tumezinduana mara kadhaa kuwa njia tunayokwenda siyo na kuelekezana na kuonyeshana
njia iliyo bora lakini tumezama katika siasa na migogoro kiasi ambacho hakuna tofauti ya jana na leo, ya
mwanasiasa wa miaka ya miaka ya kupigania uhuru na yule wa nusu karne baada ya uhuru huo.
Imesemwa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa Chama cha Upinzani Seif Shariff
Hamad kuwa miongo sita ya siasa za Zanzibar hazijaweza kabisa kupata
muwafaka wa kitaifa na kwa hivyo tokea kuja siasa Zanzibar hadi leo ni
mivutano ya kisiasa
Kwa wengi mivutano hiyo ya kisiasa na migogoro inayozalishwa ndio chanzo
kikuu cha kudumaa Zanzibar kiuchumi, kukosekana mshikamano ndani ya
nchi lakini baya zaidi kwa Zanzibar ni kupoteza mamlaka yake kwenye picha
kubwa ya Muungano wa Tanzania.
Kabla hatujaenda kuitizama migogoro ya Zanzibar ni ipi katika kipindi cha
uhai wake wote, ni muhimu kutizama vyanzo vya migogoro katika jamii na
mazingira yoyote yale ya kijamii-kiuchumi, ambayo pia ndio hayo yaliopelekea
Zanzibar kuingia katika jakamoyo hilo.
Kwa maana nyengine migogoro ni matokeo ya matukio ya kijamii na kiuchumi
na wala si kitu ambacho mtu angeweza kupigana nacho au kupingana nacho,
ila ingewezekana kama inavyowezekana sasa kujipanga vizuri zaidi katika
kupunguza nguvu zake na athari zake.
Wataalamu wa siasa wanasema kuwa vyanzo vya mizozo ya kisiasa ni vinne
ambavyo hivyo pia vinaweza kuchambuliwa zaidi katika maeneo mengine
madogo madogo, ambayo udogo huo hata hivyo usifanywe kuwa ni dhaifu
kwa maana unaweza peke yake kuripuka na kuwa ni tatizo.
Vyanzo hivyo vikuu ni:
1. Mamlaka
2. Rasilmali
3. Utambulisho wa kijamii
4. Mila
5. Utambulisho
Hatuna haja, kwa madhumuni ya makala hii kwenda ndani kuchambua kila
chanzo katika vyanzo hivyo ila itoshe tu kusema kuwa kuchapuka kwa vyanzo
vyote hivyo bila ya shaka kutategemea sana pia na kiwango cha uhuru kiliopo,
kiwango cha elimu kiliopo na pia kiwango cha ustaarabu uliopo.
Kwa maana nyengine ijapo kunaweza kuzuka kinyangan’ngyiro cha madaraka au
uwaniaji wa rasilamali basi hali inaweza kulalia upande mmoja kutoka na jinsi
watu walivyo huru kuzungumzia tatizo lilojitokeza, au uwezo kwa elimu ya
kulielewa tatizo hilo lakini pia kuwepo na utamaduni wa kuheshimu maoni ikiwa ni
sehemu ya ustarabu.
Katika hali kama hiyo basi suluhu inaweza kupatikana na tofauti hiyo isipande
daraja na kuwa ni mgogoro kwa kujua kuwa sio kila tofauti inaishia kuwa ni
mgogoro kwa maana tofauti nyengine kwa mfano za kisiasa hutolewa upepo na
kupatikana mstari wa kati mapema kabisa kabla ya kuwa mgogoro.
Nahisi kuwa nina mawazo ambayo pengine wengi wa Wazanzibari wenzangu hawana katika suala zima la kutizama
ni ipi migogoro ya Zanzibar na ambayo imetusimamia mpaka leo na kutukwamisha katika juhudi zetu mbali mbali za
kujikwamua kadri tunavyojaribu.
Kwangu mimi vyanzo vikuu vya siasa za migogoro Zanzbar naona ni hii
vifuatayo:
= Dhana ya utumwa
= Ukubwa wa dini ya Kiislamu na udogo wa Ukristo
= Majeraha wakati wa mapambano ya uhuru
= Uhuru wa 1963
= Mapinduzi ya 1964
= Muungano wa Tanzania
Najua mawazo haya yatazusha ukinzani miongoni mwetu kwa sababu wengi
watauliza baadhiya mambo lakini najua kwa yakika kwa baadhi ya mambo
hawatauliza.
Kwa mfano wengi wetu tunajua matumizi matumizi ya dhana ya utumwa
yalivyokuwa na yanavyoendelea kuwa hadi leo na kwa kiasi kikubwa
kuikwamisha Zanzibar ilhali wapo wenzetu wamechana na hilo na
wamesonga mbele kiasi kikubwa.
Dini ingawa haiku wazi sana kwa jinsi ya mazingira yake, lakini ina mchango mkubwa katika kujenga misingi
ya ugomvi wa kisiasa na hatimae migogoro kwa sababu ya wivu ambao hausemwi wazi wazi lakini
unaopepewa si kwa ajili ya vyeo lakini kupata ushawishi.
Uhuru wa Zanzibar nao. Nusu kwa nusu ya Wazanzibari wamegawika kuhusu
suala hili. Wakati ukweli wa historia tukio hilo lilitokea upande mmoja
ukisema, upande mwengine unalikataa hilo katika uhalali wake. Kukataa au
kukubali hilo kuna mambo mengine mengi ndani ya suala hilo ambayo
yanajenga tofauti za msingi baina ya Wazanzibari.
Tulisahau na hadi leo hatujawahi kutizama mvutano huo kuwa ulitokana na
mbinu za Wakoloni ambao wakati wakitoa uhuru walifanya kwa makusudi
kugawa watu na kuunga mkono vyama walivyovipendelea. Tulikuwa tupate
funzo kuwa hilo lisitutenganishe na kuwa ni jambo la mpito.
Hali kama hiyo ilitokea katika mfano halisi huko Congo wakati wa kukaribia
uhuru:
Uhuru wa Congo ulijawa kwa kiasi kikubwa na matakwa
ya Ukoloni Mamboleo. Kuelekea mkesha wa uhuru, Wabelgiji
waliaandaa mikakati ambayo ingebeba vyama walivyovipenda na pia vyama ambavyo vilivyoungwa na
makampuni makubwa ya madini ili kushinda uchaguzi na kushika serikali
Na hivi leo tukiwa tunatafuta suluhu ya kitaifa basi bado matukio
yanayotokana na kutokubaliana katika suala hilo yanaendelea kuitesa nchi hii
sawa sawa na suala zima la Mapinduzi ya 1964.
Wakati si wengi wanaohoji uhalali wa Mapinduzi ya 1964, maana si rahisi kuhoji uhalali wa Mapinduzi yoyote
yale, Wazanzibari wamegawika katika mtizamo wa juu ya madhumuni yake na hasa utekelezaji wake hasa
katika miaka yake ya mwanzo.
Kwa kiasi kikubwa Mapinduzi yamekuwa yakiungwa mkono, ingawa siku za
mwanzoni mitizamo kinzani ya siasa, wakati vyama vilivyopigwa marufuku
wenyewe walikuwapo hali ilikuwa ngumu, wengi wanahoji juu ya Mapinduzi
hayo kuhusika katika maonevu na nguvu nyingi kwa muda mkubwa kuliko
ilivyohitajika.na hivyo watu kadhaa kudhulumiwa bila ya sababu ya Mapinduzi.
Mgogoro mkubwa unaohusu Mapinduzi kwa baadhi ya watu ni kule
kushindwa kwake kupiga mstari na kuanza Zanzibar mpya yenye usawa wa
kila hali kutokana na mambo ambayo Zanzibar ilipitia na kujenga
migawanyiko.
Ndio wengine wakawa na mawazo kwamba lazima kungekuwa na wakati ambao Zanzibar ingekuwa na mfumo
wa usuluhishi wa jamii yake bila ya kujali ungepewa jina gani au ungeiga mfano wa wapi.
Kisha kuna Muungano. Muungano umesaidia sana kuibua migogoro mingi
ndani ya Zanzibar kutokana na jinsi ambavyo ushirikiano huo umekuwa
ukionekana kuwa si wa usawa na haki kwa upande mmoja.
Matukio ya karibuni kama Zanzibar Si Nchi, suala la nishati ya petroli ni moja
ya mambo mengi mno ambayo Zanzibar imepitia katika mgogoro wa muda
mrefu wa Muungano, ambapo wengi wa Wazanzibari wamegawanyika katika
ukweli wa kuukataa na unafiki wa kuukubali.
Kutokea kwa fursa mpya
Kwa miaka yote kuanzia 1964 hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa kwanza wa
Zanzibar 1995 sikumbuki kutokea au kutengezwa fursa yoyote ile ya
kusawazisha migogoro ambayo imekuwa ikiandama Zanzibar na ambayo
kuendelea kuwepo kwake kumeshindwa kuipata Zanzibar yenye utulivu wa
kisiasa.
Upande uliokuwa na mamlaka ya kufanya hivyo yaani Serikali haukupenda
kufanya hivyo kwa sababu kulikuwa na manufaa na hali hiyo kwa maana ya
kuendelea kushika madaraka katika jamii ambayo imegawika na kutawanyika
na iso na umoja.
Kwa upande wa vyama vilivyokuwa madarakani kuanzia kile cha Afro Shirazi 1964 hadi 1977 ilipokuja CCM
na CCM yenyewe kuanzia 1977 hadi 1995 pia vilifaidika na mgawiko mkubwa wa kiitikadi uliogawa pande
kuu mbili za siasa za Zanzbibar lakini navyo vyama hivyo pia vilikuwa vizito kutafuta suluhu ya kitaifa kwa
sababu ya kufaidika na hali hiyo.
Kwa upande mwengine hata Serikali ya Muungano nayo kwa kiasi kikubwa
ijapo haikuwa ikishabikia siasa za Zanzibar na migogoro yake wazi wazi lakini
tabaan ilifaidika nayo kwa kuwa Zanzibar dhaifu inatawalika rahisi na
inapunguzika madaraka rahisi.
Hata ilipobidi kuingilia kati baada ya machafuko makubwa ya kiuchaguzi ya
1995, 2000 na 2005 Serikali ya Muungano ilichukua hadhari mno kuingia na
kutafuta suluhu na wengi walikuwa na mawazo kuwa ilikuwa ikiburura miguu
na muda mwingi iliogopa kutoa kauli yenye uthabiti kuiambia Serikali ya
Zanzibar juu ya wajibu wake wa kumaliza siasa za migogoro.
Kama wasemavyo Waswahili kuwa kheri hutokana ndani ya tumbo la shari
na ndivyo ilivyotokea fursa ya kwanza ya suluhu ya Zanzibar baada ya
hasama kubwa ya Uchaguzi Mkuu wa 1995 lakini fursa yenyewe ikija mwaka
wa nne wa utawala wa Rais Salmin Amour baada ya Jumuia ya Madola
kusaidia katika hilo.
Ni pale tunaweza kusema kuwa mchakato wa kuitafuta Zanzibar mpya
ulianza. Palipatikana mafanikio kidogo, lakini kwa sababu wahafidhina na
wale wanaendelea kutizama suala la siasa na migogoro Zanzibar katika
vyanzo vikuu vile 6 nilivyovitaja na kutokuwa tayari kubadilika, walizuia
mabadiliko yasisonge mbele.
Na ndipo tulipoingia katika Uchaguzi Mkuu wa 2000 ambao sina haja ya
kutaja athari zake lakini ningependa kutaja mafanikio yake baada ya
Muwafaka wa 2001 ambapo hatua nyingi zilichukuliwa na kutandika misingi
mizuri zaidi ya kuelekea katika zama mpya za Zanzibar. Bado wahafidhina na
wanaoshikilia siasa za migogoro Zanzibar katika misingi ile 6 wakabakia na
ushupavu wao, ingawa walianza kupungua.
Uchaguzi wa 2005 ukawa vile vile wa utata, na bado tukaingia katika
mazungumzo mengine tena ya kutafuta Muwafaka na mazungumzo hayo
yakakwama tena katika dakika za mwisho na sina haja ya kusema kuwa
yalikwamisha tena na wale wale amboa ni kundi lenye mtizamo wa
kihafidhina na lisilotaka kuondoka katika hiyo misingi 6 niliyoitaja.
Mazungumzo ya miezi 14 yakabomolewa kwa kikao kimoja tu na kauli za
watu wachache tu ambao wanaamini wanawasemea wengi kwamba mawazo
ya Wazanzibari hayaweza kuja pamoja na kuwa tofauti zao haziwezi
kusuluhishika na kuwa hawawezi kufanya kazi pamoja.
Mpaka mwishoni mwa mwaka jana. Na yaliotokea Novemba 5, 2009 sasa
yameshaanza kuwa sehemu ya historia. Zanzibar katika fursa hii mpya
imepiga hatua ambayo ilikuwa ikitafutwa na kuhitajika kwa miaka 46 lakini
kwa miezi michache tu kila mlango wa fursa hiyo umefunguka kana kwamba
haukuwa umefungwa kwa lakiri.
Fursa mpya imenza kuzaa zama mpya.
litaipeleka nchi hii katika zama mpya na fikra mpya na Zanzibar yenye sauti
na fursa ya kila mmoja.
Mwisho
Marejeo
Abdul - Raheem, T., (ed), 1996, Pan-African Politics, Economy and Social
Change in the Twenty-First Centuary; Kampala: Pluto Press.
Mpangala, G, Conflicts and Peace Building in the Great Lakes Region
-www.grandlacs.net