Professional Documents
Culture Documents
YEREMIA 29:11
"Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema BWANA, ni mawazo ya amani, wala si ya
mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho"
Kila kitu kinachoonekana kwa macho katika ulimwengu huu wa kuonekana (hasa kilicho
sababishwa na binadamu) ni matokeo ya wazo au mawazo yaliyo ndani ya mtu (binadamu).
Kwa mfano, nyumba/jengo ambalo linaweza likawepo mahali fulani lilitokana na wazo
lililokuwa ndani ya fikra za mtu. Hapo mwanzo mtu alipendelea kuwa na nyumba ya namna au
mtindo fulani. Wazo hilo likahamishwa na fundi msanifu majengo (architect) na kuwekwa kama
mchoro kwenye karatasi na kujulikana kama ramani ya jengo. Baada ya hapo mjenzi wa nyumba
(contractor) akaichukua na kuutumia mchoro huo kujenga nyumba/jengo lenye kutumika kama
kitu halisia chenye manufaa kwa binadamu. Hivyo nyumba imekuwa kitu dhahiri chenye
kushikika ambacho asili yake ni wazo lililokuwa ndani ya kichwa cha mtu (akili za mtu).
Hivyo kuwepo kwa jengo hilo kuna maanisha kuwa mawazo au wazo la jengo lililokuwa ndani
ya fikra ya mtu hapo awali, limekuwa dhahiri (materialized/made into reality).
Hakuna mtu anayefika juu sana katika kusafiri kimaisha kama hakuwahi kufikiri na kuwa na
maono hayo ya kuja kufika huko juu (viwango vya juu).
Kwa upande mwingine inakuwa ni bahati nzuri sana kwa jamii yoyote ile kuwa na mtu au watu
wenye mawazo chanya. Mawazo yenye kuleta faida katika jamii, mawazo ambayo
yanapofanyiwa utekelezaji, basi yanazalisha faida na si hasara katika jamii.
Mawazo ya mtu hudhihirika kupitia kinywa cha mtu mwenyewe (muwazaji). Kwa mfano, watu
wengine huwatukana watoto wao kwa kusema “mjinga wewe, huna akili wewe,” sasa hayo ni
maneno hasi yanayotoka katika kinywa cha mtu mwenye mtazamo hasi. Mtoto huyo anaenda
kuwa mjinga tu na hatakuwa na akili kwa sababu kutoka katika kinywa tunaweza kuumba au
kusababisha matokeo chanya au hasi. METHALI 18:21
Kinywa hicho kina uwezo wa “kumloga” mtu mwingine kwa njia ya kutamka tu. Wengine
wamewaloga watoto wao kwa kuwatamkia maneno mabaya ambayo yameenda kufanya kazi ya
kuharibu maisha ya mtoto huyo. Huo ni mfano tu ulio hai hasa kwa familia nyingi za kiafrika.
Ni muhimu kutambua kuwa hatari ya kiumbe huyu anayeitwa “binadamu” ipo katika mdomo, na
usalama na uhai upo katika mdomo huo huo. Hii ndio maana wapo watu waliofungwa jela (kwa
kukosea kisheria) kwa sababu ya kukosea kusema au kumtukana (kumkashifu) mtu mwingine…
ndio maana imetolewa onyo katika maandiko MATAYO 12:36-37.
Hatari na usalama unatoka katika kinywa cha mtu. Ndio maana kwa kutumia kinywa mtu
anaweza kuwa tajiri (METHALI 18:21) kwa sababu ya nyimbo anazoimba na watu kuburudika
na kufarijika hata kuwa tayari kulipa kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya kununua au kugharamia
ili wasikie sauti ya mwimbaji huyo.
Kinywa kikitumika vibaya kinauwezo wa kuharibu mambo mazuri ambayo jamii ingependa
yaendelee kuwepo (kufanyika). Hii ndio maana kipo kikundi Fulani chenye mlengo wake katika
taifa Fulani kilichozuiliwa hata kufanya mikutano ya hadhara kwa sababu wao badala ya
kujenga, wanabomoa. Badala ya kusisitiza mshikamano wa kitaifa katika kuwaletea maendeleo
wananchi, wao ndio wanapandikiza mbegu ya chuki na kutafuta madhaifu ya walioshika hatamu
ili kutibua harakati za kujenga uchumi.
Kinywa kina nguvu isiyo ya kawaida ndio maana Tanganyika walimuondoa mkoloni kwa
maneno tu pasipo kutumia mtutu wa bunduki. “Sauti inaweza kumtoa nyoka pangoni”… Je
wewe unaitoa sauti (maneno) yako kwa lengo gani? Ni sauti iliyo kero kwa watu au burudani au
kivutioa au yenye kuleta hamasa ya mshikamano au yenye kukatisha tamaa watu katika maono
yao ya kuendelea?